PEPEA RADIO
Sauti ya Afrika
Sauti ya Afrika
VITA baridi vya kisiasa kati ya Rais William Ruto na aliyekuwa Naibu wake Rigathi Gachagua viliendelea hadharani jana wawili hao wakikosa kusalimiana walipokutana katika hafla ya kanisa kaunti ya Embu.
Wawili hao walihudhuria hafla ya kutawazwa kwa Askofu Peter Kimani Ndung’u wa dayosisi ya Kanisa Katoliki iliyofanyika katika Chuo Kikuu cha Embu.
Hii ilikuwa mara ya kwanza wawili hao kukutana tangu Bw Gachagua alipotimuliwa ofisini mwezi jana.
Katika hafla hiyo, Rais Ruto na Bw Gachagua hawakusalimiana, ikionyesha wazi tofauti zao za kisiasa zinaendelea.
Hata hivyo, Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta ambaye alifika baada ya Rais Ruto alichangamkiwa na waumini na viongozi waliohudhuria.
Waumini waliojawa na furaha walimshangilia Bw Kenyatta kwa sauti kubwa alipokuwa na kutatiza sherehe hiyo kwa muda.
Ilibidi Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Anthony Muheria ambaye kuwakumbusha waumini kuwa walikuwa katika ibada ya Kanisa na walipaswa kunyamaza.
Bw Gachagua alifika mapema kabla ya Dkt Ruto na kuketi miongoni mwa waumini na kufuatilia sherehe
Hata hivyo Rais Ruto alipofika, Bw Gachagua hakusonga kukutana naye kumsalimia.
Wawili hao walikaa umbali mdogo kutoka kwa kila mmoja, lakini hawakupeana mikono hata kidogo.
Lakini Bw Kenyatta alikaa karibu na Prof Kindiki lakini hakushiriki mazungumzo naye au kiongozi wa nchi wakati wote wa hafla hiyo ambayo ilivutia mamia ya waumini, maaskofu na viongozi kote nchini.
Bw Kenyatta pia hakusalimiana na Bw Gachagua. Kabla ya kuondolewa mamlakani, Bw Gachagua aliashiria alikuwa amezika tofauti zake na Bw Kenyatta akisema alitumiwa kumshambulia wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa 2022 na punde baada ya kuingia mamlakani.
Washirika wa Rais Ruto Gavana Cecily Mbarire, Seneta wa Embu, Alexander Mundigi, Mbunge wa Embu Kusini Nebart Muriuki, Mbunge wa Runyenjes, Eric Muchangi na Gitonga Mukunji wa Eneo Bunge la Manyatta walihudhuria.
Gavana Mbarire aliketi kando ya Dkt Ruto na wawili hao wakaendelea kuzungumza.
Hakuna kiongozi wa kisiasa aliyemtambua Bw Gachagua katika hafla hiyo isipokuwa viongozi wa kidini ambao walishangiliwa na umati walipotaja jina lake.
Gavana wa Embu Cecily Mbarire ambaye alikuwa mwenyeji, alimwalika Kindiki kuhutubia waumini, ambaye alimwalika Uhuru Kenyatta, kisha Kindiki akarudi jukwaani kumwalika Rais Ruto kukamilisha itifaki kabla ya hafla kukabidhiwa tena kwa Askofu wa Kanisa Katoliki. Peter Ndung’u.
Wakati wa hotuba zao, Bw Gachagua alikaa kimya akatazama maafisa wakuu wa serikali wakizungumza.
Muda mfupi baada ya hafla hiyo, Gachagua, akiandamana na washirika wake wa kisiasa Mlima Kenya akiwemo Mbunge wa Githunguri Gathoni Wamuchoba waliondoka licha ya mwito wa baadhi ya waumini kumtaka ahutubu.
Baada ya kuondolewa mamlakani, Bw Gachagua alivuliwa wadhifa wa naibu kiongozi wa chama ambao ulikabidhiwa mrithi wake Kithure Kindiki ambaye alihudhuria hafla ya jana.
Haya yanajiri huku ikisemekana Bw Gachagua na Bw Uhuru wanasuka muungano kwa lengo la kupunguza ushawishi wa Rais Ruto katika eneo la Mlima Kenya.
Aliyekuwa Gavana wa Kiambu Ferdinand Waititu, mkosoaji mkubwa wa serikali ya Rais Ruto alikuwa kwenye hafla hiyo lakini aliketi miongoni mwa waumini.
Rais Ruto aliwahakikishia Wakenya kuhusu kujitolea kwake kuhakikisha Hazina ya Bima ya Afya ya Jamii (SHIF) inafanya kazi kwa manufaa ya Wakenya wote.
Mkuu wa Nchi alisema amepokea malalamishi ya Kanisa na Wakenya na akaahidi kusuluhisha matatizo ya SHIF yanayowakabili wananchi.
‘Makosa yaliyobainishwa na kanisa Katoliki katika SHIF yatarekebishwa, nataka kuhakikisha kuwa huduma za afya sio za matajiri. Utoaji wa afya kwa wote utaleta mabadiliko na hakuna Mkenya atakayeachwa nje,’ alisema Dkt Ruto.
Rais alisema Mtaala unaozingatia Mtaala (CBC) unafaulu na kuwataka Wakenya kuwa na subira na kuukumbatia.
RAIS William Ruto amemteua aliyekuwa Gavana wa Nairobi Evans Kidero na dadake kiongozi wa chama cha ODM Raila Odinga, Wenwa Akinyi kuhudumu katika nyadhifa serikalini.
Dkt Kidero ameteuliwa kuwa mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi ya Shirika la Kitaifa kuhusu Biashara Kenya (KNTC) kwa muda wa miaka mitatu.
Katika kumteua Dkt Kidero, Rais alibatilisha uteuzi wa Hussein Debasso. Dkt Kidero amekuwa kwenye baridi baada ya kushindwa katika kinyang’anyiro cha ugavana wa Homa Bay katika Uchaguzi Mkuu wa 2022.
Mwaka jana, Dkt Kidero alikuwa miongoni mwa watu ambao Rais Ruto aliteua kuwa Mawaziri Wasaidizi kabla ya uteuzi huo kufutiliwa mbali na mahakama.
“Namshukuru Mheshimiwa Rais Ruto na ninaahidi kutoa huduma kwa kujitolea kwa watu na taifa la Kenya Ili kuongeza thamani na kuleta mabadiliko,” Dkt Kidero alisema kufuatia kuteuliwa kwake.
Katika uteuzi wa hivi punde kupitia notisi ya gazeti la serikali ya Novemba 15, 2024, Rais pia alimteua Dkt Wenwa kuwa Mwenyekiti wa Taasisi ya Utafiti wa Bahari na Uvuvi ya Kenya, kwa muda wa miaka mitatu.
Rais Ruto pia alimteua Dkt Thuo Mathenge kuwa mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Utafiti wa Kilimo na Ufugaji kwa miaka mitatu kuchukua nafasi ya Peter Weru Kinyua ambaye uteuzi wake ulibatilishwa.
MAKUNDI mawili ya kutetea haki za kibinadamu yameiandikia Safaricom kufuatia ripoti kuwa kampuni hiyo ya mawasiliano imekuwa ikitoa data za wateja wake kwa maafisa wa usalama kuwasaidia kusaka na kuteka nyara washukiwa.
Katika barua yao kwa Mkuu wa Kitengo cha Sera za Umma na Usimamizi wa kampuni Fred Waithaka, Tume ya Kutetea Haki za Kibinadamu Nchini (KHRC) na Kundi la Waislamu kuhusu Haki za Kibinadamu (Muhuri) yalitaja ripoti iliyochapishwa katika gazeti la ‘Daily Nation‘ Oktoba 29, ilionyesha jinsi Safaricom imekuwa ikitekeleza uovu huo.
Makundi hayo ya kutetea haki yaliilaumu kampuni hiyo ya mawasiliano kwa kupeana data kwa maafisa wa polisi “wenye sifa mbaya ya kutumia mbinu haramu kupambana na washukiwa ikiwemo kuwaua.”
Ingawa Safaricom ilitoa taarifa mnamo Oktoba 31, 2024 ikifafanua kuhusu madai hayo, KHRC na Muhuri zinasema taarifa hiyo haikujibu moja kwa moja yale yaliyofichuliwa kwenye uchunguzi huo.
Kwa misingi hiyo, makundi hayo ya kutetea haki za kibinadamu yanaitaka Safaricom kujibu orodha ya madai saba ya “kuchukiza” yaliyotolewa kwenye ripoti ya Daily Nation.
KNHR na Muhuri zilisema kuwa Safaricom inapopewa agizo la mahakama kwamba itoe rekodi za data kuhusu mawasiliano ya simu zinazoweza kuwahusisha maafisa wa usalama na maovu kama mauaji ya kukusudia, hupitisha wajibu huo kwa kitengo cha polisi cha ushirikishi wa umma.
“Hii huleta hali ya mgongano wa kimasilahi kwa kuwapa maafisa wa kitengo kinachotuhumiwa nafasi ya kupata data na kuficha ushahidi kuhusu uhalifu na hatima ya waathiriwa,” mashirika hayo yanasema.
Aidha, yanahoji ikiwa Safaricom ilitoa data ambazo ilithibitisha kuwa halali licha ya kuonyesha dalili kwamba zilivurugwa.
KNHR na MUHURI zinaitaka Safaricom kuthibitisha ikiwa hutoa kwa maafisa wa usalama rekodi hizo za data baada ya kupokea agizo la mahakama kutokana na kesi zinazohusu visa vya watu kutokomezwa na serikali kwa nguvu.
Kwa kukataa kila mara kutoa data muhimu kusaidia katika uchunguzi wa maovu yanayotendwa na serikali nchini Kenya, hata baada ya kupokezwa maagizo ya mahakama, KHRC na MUHURI zinailaumu Safaricom kwa “kuhujumu haja ya kupatikana kwa haki.”
Mashirika hayo pia yanaitaka Safaricom itoe maelezo kuhusu madai kuwa iliruhusu asasi za usalama kupata data za wateja wake hata bila agizo la mahakama, na hivyo kusaidia katika kusaka na kukamatwa kwa washukiwa.
KHRC na MUHURI pia zinataka kampuni hiyo ya mawasiliano kutoa maelezo kuhusu madai kuwa imehifadhi data za “zamani” inazodai ilifuta, zikiwemo data ambazo zinaweza kusaidia katika uchunguzi wa uhalifu uliotekelezwa na serikali.
Mashirika haya mawili pia yanaitaka Safaricom kufafanua kuhusu madai kuwa, pamoja na kampuni ya Neural Technologies Limited, ilitengeneza programu inayowezesha vikosi vya usalama nchini Kenya kupata data za kibinafsi za wateja wao. Na data hizo ndizo zimetumika na maafisa.
JUMLA ya vifo sita vinavyohusiana na ajali za baharini vilirekodiwa kaunti ya Lamu mwaka huu, 2024.
Vifo hivyo vilifuatia ajali 17 za baharini zilizoripotiwa kati ya Januari na Novemba mwaka huu.
Visa hivyo vilihusisha boti na mashua kuzama baharini baada ya kusombwa na mawimbi makali, vyombo vya baharini kulipuka na kushika moto au kupasuka katikati na kuzama vikiwa katikati ya bahari, kufeli kuogelea kwa baadhi ya watu wakijivinjari baharini, vyombo kupotea na kisha mabaharia kupatikana wamekufa maji kwenye Bahari Hindi Lamu.
Kuna visa ambapo mashua na boti ziliripotiwa kutoweka baharini, ambapo shughuli za kusaka vyombo na mabaharia hao ziliendelezwa hadi kusitishwa baada ya wahusika kukosekana.
Katika mahojiano na Taifa Dijitali, Mkurugenzi wa Idara ya Majanga na Uokoaji wa Dharura, Kaunti ya Lamu, Bw Shee Kupi, alikiri kupungua kwa idadi ya majanga ya baharini yaliyorekodiwa 2024 ikilinganishwa na mwaka uliopita.
Aidha idadi ya vifo vya baharini viliongezeka mwaka huu ikilinganishwa na mwaka jana, 2023.
“Mwaka huu tulirekodi visa 17 vya majanga ya baharini ambapo juhudi zilifanywa na wahusika kuokolewa. Ila tulipoteza watu 6. Mwaka jana, 2023, tulirekodi visa 22 vilivyoripotiwa, ambapo waliofariki ni 5, wengine wakiokolewa,” akasema Bw Kupi.
Kwa mujibu wa kitengo hicho cha idara ya majanga ya baharini, dhoruba kali ilishuhudiwa mwaka 2023 kwenye Bahari Hindi ilhali mwaka 2024 kukishuhudiwa utulivu wa hali ya juu, hivyo kuongeza usalama kwa wasafiri wa majini.